Social Icons

Wednesday 3 August 2016

Mwanafunzi Udom auawa kwa kipigo

MWANAFUNZI wa mwaka wa kwanza Kitivo cha Sayansi ya Jamii katika Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) Fredrick Joseph (25), ameuawa kwa kushambuliwa kwa kipigo na watu wanaosadikiwa kuwa ni wanafunzi wenzake.
Tukio hilo ni la juzi usiku katika eneo la chuo hicho, ambapo mwanafunzi huyo alisikika akipiga kelele, ndipo walinzi wakafika na kumkuta akiwa anagalagala njiani.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa, alisema mwanafunzi huyo alishambuliwa kwa kupigwa sehemu mbalimbali za mwili wake na watu wasiofahamika.
Alibainisha kuwa mwanafunzi huyo alikutwa majira ya saa 10 alfajiri katika eneo hilo la chuo. Hata hivyo, alisema uchunguzi wa awali umebaini kuwa mwanafunzi huyo alikuwa na ugomvi na watu hao katika klabu ya pombe ya Canival Pub iliyopo chuoni hapo.
“Alipoondoka kurudi bwenini akiwa njiani alishambuliwa na watu hao wasiofahamika na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake, kipigo kilichosababisha kifo chake wakati alipokimbizwa kutibiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Dodoma,” alisema Mambosasa.
Alisema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika hospitali hiyo kwa uchunguzi zaidi na hadi sasa hakuna mtu anayeshikiliwa kuhusiana na tukio hilo. Kamanda huyo alisema ameelekeza uchunguzi wa kina ufanyike kuhusiana na ugomvi huo ili kubaini wahusika.
Wakati huo huo, mkazi wa Kondoa, Amlan Mabata (54) anadaiwa kujinyonga kwa kutumia kamba ya manila juzi saa 12 asubuhi kwenye mti jirani na Gereza Kuu la Isanga Dodoma.
Alisema chanzo cha kujinyonga ni ugomvi wa kifamilia kati yake na hawara yake, ambaye ni askari magereza wa gereza hilo. Kamanda Mambosasa alisema Jeshi la Polisi linamhoji askari huyo.

CHANZO HABARI LEO

No comments: