Social Icons

Tuesday 18 August 2015

Mfumo mpya wa elimu sasa wapendekezwa.

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. Tumieni mtandao huu ni wenu nyote.
  Kuna makadirio ya watanzania milioni 23 kwenye soko la ajira.
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue.
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue (pichani), amesema ingawa kuna Sera ya Elimu, lakini kuna haja ya kuunda upya mfumo wa elimu nchini ili uendane na hali ya uchumi wa sasa wa dunia pamoja na upatikaji wa ajira kwa vijana nchini.
 
Alisema kwa sasa kuna tatizo kubwa la upatikanaji wa ajira nchini kunakosababishwa na ukosefu wa ujuzi wa maendeleo, huku zaidi ya watafuta ajira 800,000 kutoka nje ya nchi wakiingia nchini kutafuta ajira kila mwaka.
 
Aliyasema hayo jijini Dar es Salaam wakati akifungua warsha ya kuandaa mkakati wa kitaifa wa kujenga na kuimarisha stadi za kazi katika sekta zinazochochea ukuaji uchumi , iliyowakutanisha baadhi ya makatibu wakuu nchini. 
 
Alisema kwa sasa nchi inahitaji mfumo wa elimu ambao utawasaidia vijana kupata ajira kwa urahisi kwa kuwa tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana linazidi kukua siku hadi siku na kuhatarisha uchumi wa nchi.
 
Aliongeza kuwa ingawa uchumi unakua kwa wastani wa asilimia sita hadi saba kwa mwaka tangu miaka kumi iliyopita, lakini ukuaji huo haujasaidia upatikanaji wa ajira ya uwakika kwa vijana wanaomaliza masomo vyuoni.
 
“Leo kuna makadirio ya Watanzania milioni 23 kwenye soko la ajira, na idadi hiyo inakisiwa kuongeza hadi kufikia milioni 45 ifikapo mwaka 2030, na ongezeko la watu linakua kwa kasi kwa milioni 1.2 kwa mwaka, hivyo tusipokuwa makini tutatengeneza kizazi kisicho kuwa na elimu,” alisema Sefue.
 
Aliongeza kuwa taasisi za elimu nchini hususani vyuo vikuu wanawapatia wanafunzi ujuzi ambao hauendani na soko la ajira ama elimu ambao haiendani na nini soko la ajira duniani linahitaji.
 
Alisema taasisi za elimu zinapaswa kuboresha masomo kwa wanafunzi wao ambayo yataendana na soko la ajira pamoja na kuinua uchumi wa nchi utakaosaidia kuwavutia wawekezaji kwa wingi 
 
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF),  Godfrey Simbeye, alisema Serikali na sekta binafsi zinapaswa kufanya kazi kwa pamoja ili kutatua tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana kwa kutengeneza sera madhubuti zitakazo okoa tatizo hilo.
 
Alisema kwa kuwapo kwa sera ya maendeleo ya ujuzi katika elimu kutasaidia kuwaongezea vijana ujuzi wa kufanya kazi pindi wawapo katika masomo na kuutumia ujuzi huo watakapokuwa wakitafuta ajira ama wakishaajiriwa.
CHANZO: NIPASHE

No comments: