Social Icons

Monday 29 September 2014

JAMII YAASWA KUCHANGIA MAENDELEO YA ELIMU.


Na. Aron Msigwa –MAELEZO.
28/9/2014. Dar es salaam.

Wahitimu wa vyuo mbalimbali nchini wameaswa kujenga utaratibu wa kuchangia miradi na shughuli mbalimbali za maendeleo ya elimu katika vyuo walivyosoma na kuepuka kutumia fedha nyingi katika kuchangia masuala yasiyo na tija kwa maendeleo ya taifa.

Hayo yamebainishwa jana jijini Dar es salaam na mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara Dar es salaam (CBE) Prof. Emanuel Mjema , wakati wa hafla ya kuwakaribisha chuoni hapo waliokuwa wanafunzi wa chuo hicho waliohitimu miaka iliyopita kwenye mwendelezo wa maadhimisho ya  miaka 50 ya chuo hicho.

Akizungumza na wahitimu hao amesema kuwa wanayo nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko katika sekta ya elimu hapa nchini kwa kushiriki na kutumia sehemu ya mapato wanayopata kupunguza changamoto za elimu za uhaba wa vyumba vya madarasa, maabara na miundombinu mingine isiyo rafiki kwa maendeleo ya wanafunzi. 

“Elimu ndio msingi wa maendeleo, sisi tulipata elimu iliyo bora lazima tuchangie kwa sehemu yetu kuonyesha tunayajali maeneo tuliyosoma, hivi sasa mwamko wa  watu wengi uko katika kuchangia sherehe na harusi lakini kwenye suala la elimu hali ni tofauti” Amesema Prof. Mjema.

Amesema wahitimu hao wana nafasi kubwa ya kuendelea kuwa mfano kwa kuendelea kutoa mrejesho kwa uongozi juu ya nini kifanyike katika kuendeleza sekta ya elimu chuoni hapo sanjali na  kueleza mapungufu yaliyopo pamoja na kutoa michango yao juu ya namna ya kuendeleza kiwango cha taaluma.

Amebainisha kuwa chuo hicho kinahitaji kiasi cha shilingi bilioni 3 ili kiweze kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo ya upanuzi wa kampasi zake, ujenzi wa miundombinu,uongezaji wa vifaa vya kufundishia, madarasa, maabara na kumbi za mihadhara.

Kwa  upande wake Bw. Alexander Msofe akizungumza na wahitimu hao kwa niaba ya Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo hicho ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi katika  hafla hiyo amesema chuo hicho kinafurahia matunda ya mafanikio ya kutimiza miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.

Amewaambia wahitimu hao kuwa licha ya changamoto mbalimbali zinazokikabili chuo hicho kimeweza kuongeza idadi ya wanafunzi  wanaodahiliwa  kwa mwaka kutoka 25 waliodahiliwa mwaka 1965  hadi 14,000 katika mwaka wa masomo wa 2014/15 pamoja na ongezeko la  idadi kozi za masomo zinazotolewa kutoka 1 hadi 6. 

Bw. Msofe ameongeza  kuwa chuo cha CBE sasa kinatimiza miaka 50 kikiwa chuo pekee Afrika ya Mashariki na katika nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) kinachotoa wanafunzi wa shahada ya vipimo.

Mafanikio mengine ni pamoja na kuongezeka kwa kozi za masomo na ngazi za mafunzo hadi kufikia shahada, kuongezeka kwa wakufunzi wenye shahada za uzamivu (PhD) chuoni hapo  pamoja na chuo kuanzisha ushirikiano wa elimu na vyuo vikuu vingine nje ya nchi kikiwemo Chuo Kikuu cha Eastern Finland katika utoaji wa mafunzo ya shahada za uzamivu kwa kutumia TEKNOHAMA kwa nchi za SADC.

 Aidha, katika kuelekea tamati ya maadhimisho ya chuo hicho yatakayofanyika  Januari  13, mwaka 2015 ameitaka jamii na wahitimu wote wa chuo hicho wajitokeze wingi kutoa michango yao ya hali na mali itakayowezesha ujenzi wa vyumba vya madarasa na mihadhara, maabara na vyumba vya kulala wanafunzi.
Kwa upande wao wanafunzi waliowahi kusoma chuoni hapo wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa hafla hiyo wametoa wito kwa wadau mbalimbali wenye mapenzi mema kujitokeza kuchangia ukamilishaji wa programu mbalimbali za maendeleo zilizoanzishwa na uongozi wa chuo hicho.

Wamesema kuwa badala ya kuiachia serikali pekee jamii na wahitimu hao wanayo nafasi  kubwa ya kuchangia maendeleo ya chuo hicho kutokana na wao kuendelea kufaidika na elimu waliyoipata kipindi wakiwa wanafunzi wa chuo hicho.

Wameiomba serikali kuhakikisha kuwa inaendelea kukisaidia chuo hicho na kukitumia kupata ushauri wa kufanikisha masuala mbalimbali yakiwemo mafunzo kwa wafanyabiashara na uimarishaji wa mifumo ya ukusanyaji wa kodi hapa nchini ili kuondoa tatizo la asilimia kubwa ya watu kukwepa kodi. 

Kwa wanavyuo wote watanzania popote Duniani Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. Tumieni mtandao huu ni wenu nyote.

No comments: